MAGONJWA NA WADUDU WANAOSHAMBULIA KUKU NA JINSI YA KUKINGA



Mada: Ufugaji bora wa kuku


1.      Aina za kuku wanaopatika hapa nchini Tanzania (koo za kuku), elezea aina za kuku wa kienyeji na kisasa
Kuna aina nyingi za kuku wanaopatikana hapa nchini. Kuku hawa hutambulika kutokana na maumbile yao, muonekanao na asili wanapotoka.

Kuku wa Asili
·         Kuchi – Wana miili mikubwa, miguu mirefu na ukiko wenye umbile la uaridi (rose)
·         Kishingo – Ni kuku wasio na manyoya shingoni na hii ndio asili ya jina lake. Wana miguu ya urefu wa wastani na miili ya ukubwa wa wastani
·         Tewe – Wana miguu mifupi na maumbile madogo, ni watagaji na waatamiaji wazuri
·         Bukini – Ni aina ya kuku wasio na manyoya marefu mikiani
·         Kinyafu (Njanjame) – Wana manyoya yaliyokunjamana na maumbile ya aina tofauti

      Kuku wa kisasa
Hawa wamegawanyika katika makundi makuu mawili:- Kuku wa Nyama na kuku wa Mayai

Kuku wa Nyama – Ni maarufu sana kwa ukuaji wao wa haraka na uzalishaji wa nyama kwa wingi
·         White Cornish (Ni weupe na hupatikana kwa wingi katika maeneo mbalimbali nchini)
·         White Plymouth Rock (Nao ni weupe na michirizi myeusi)

Kuku wa Mayai – Ni maarufu kwa utagaji wao wa mayai kwa wingi
·         White leghorn – Ni weupe na hutaga mayai mengi, wana maumbo madogo na hivyo huhitaji chakula kidogo
·         Rhode Island Red – Wana rangi nyekundu, kutokana na maumbo yao kuwa makubwa, wafugaji huwatumia pia kwa uzalishaji wa nyama
·         New Hampshire – Wana rangi ya kahawia (Brown) nao wana maumbo makubwa ni watagaji wazuri lakini pia wazalishaji wa nyama

2.      Taratibu za kupokea vifaranga, au kuku wakubwa kutoka kwa mzalishaji wa vifaranga, au sokoni wanapouzwa.
Siku zote mfugaji anashauriwa kutafuta vifaranga au kuku wakubwa kutoka kwa wazalishaji waaminifu ambao huzingatia kanuni za ufugaji bora ikiwepo kuzingatia ratiba zote za chanjo ili kuzuia hasara inayoweza kujitokeza kutokana na magonjwa yanayoweza kuzuilika.
Kabla ya kupokea vifaranga mfugaji anashauriwa kufanya maandalizi muhimu ikiwepo kuandaa banda au chumba cha kulelea vifaranga, ikiwemo kuhakikisha kuwa ameandaa vyombo vya chakula na maji, ameandaa chakula kwa ajili ya vifaranga, kuhakikisha kuwa joto la chumba atakacho wafugia ni la wastani kulingana na umri wao.

3.      Uleaji wa vifaranga elezea: njia ya kubuni na njia ya asili kama zipo.
Zipo njia tofauti za kulea vifaranga. Vifaranga huweza kuachwa na mama yao ili awalee au kulelewa kwa kutumia nishati. Mahitaji makubwa ya vifaranga kutoka kwa mama yao ni joto, hivyo mfugaji anaweza kuwalea vifaranga kwa kuwapatia joto kutokana na vyanzo mbalimbali kama vile taa ya chemli au jiko la mkaa. Lakini pia vifaranga huweza kulelelewa bila nishati kwa kutumia chumba kisichopitisha upepo wala baridi wakati wa mchana na kuwaweka katika boksi au kasha lilitandazwa maranda ya mbao au matambara wakati wa usiku, katika utaratibu huu, vifaranga watapeana joto wao kwa wao.



4.      Sifa za kuku bora.
Sifa za kuku bora hutofautiana kulingana na malengo ya mfugaji. Ikiwa ni kwa lengo la nyama basi aweze kuzalisha nyama kwa wingi na kama ni kwa lengo la mayai basi aweze kutaga mayai mengi. Kwa ujumla kuku bora anatakiwa kuwa na sifa zifuatazo:-
Sifa za Jogoo bora
·         Mwili mkubwa
·         Wanaokua haraka
·         Wenye bidii ya kupanda
·         Uwezo wa kuitia matetea chakula
·         Asiwe mkali kwa vifaranga
Sifa za tetea bora
·         Mwenye mwili mkubwa
·         Wanaokua haraka
·         Wanaotaga mayai mengi na makubwa
·         Uwezo mzuri wa kuatamia na kutotoa mayai mengi
·         Uwezo mzuri wa kulea vifaranga

Mada:  Mifumo ya ufugaji kuku,
 Utofauti wa ufuganji wa bandani, huria na nusu huria
Ipo mifumo tofauti ya kufuga kuku
Mambo yanayomfanya mfugaji aamuue aina ya mfumo wa kutumia katika ufugaji wake ni uwezo wake kifedha na ukubwa wa eneo lake la kufugia.
Mfumo huria
Kuku huachwa nje wajitafutie chakula na maji wao wenyewe. Mfumo huu hutumiwa zaidi na wafugaji wa kuku wa asili. Ni mara chache sana kuku kupewa chakula cha ziada na mahali pa kulala katika mfumo huu.

Faida za mfumo huria.
·         Ni mfumo rahisi ka mfugaji kwa sababu kuku hujihudumia kwa sehemu kubwa
·         Ni mfumo wenye gaharama ndogo kwa sababu hakuna gharama ya kuwapa chakula wala kuwajengea sehemu ya kulala.
·         Ni mfumo unaowawezesha kuku kupata mazoezi ya kutosha
·         Ni mfumo unaowafanya kuku kujipatia virutubisho mchanganyiko katika mazingira jambo ambalo ni zuri kiafya.

Hasara za mfumo huria
·         Kuku huwa hatarini kuibiwa, kukanyagwa na magari, kudhurika na hali mbaya ya hewa na wanyama wakali kama vicheche, mwewe nk.
·         Vifaranga wengi hufa na kupotea.
·         Kuku huharibu mimea ya bustanini na mazao mengine na hivyo huweza kusababisha ugomvi na majirani.
·         Kuku hutaga sehemu yoyote na upotevu wa mayai ni mkubwa.
·         Ni vigumu kufuatilia afya ya kuku kwa karibu na hivyo ni vigumu kutoa tiba na kinga kwa wakati.
·         Ni vigumu kutunza kumbukumbu sahihi za ufugaji.
·         Ni rahisi kuku kuambukizwa magonjwa na kuku wengine.

Mfumo wa nusu huria
Katika mfumo huu, kuku hufugwa kwenye banda lililozungushiwa uzio ili kuwazuia kuku wasiende mbali. Kuku huwa na uhuru wa kukaa aidha ndani ya banda au nje ya banda kwenye eneo lililozungushiwa uzio.

Faida za mfumo wa nusu huria
·         Kuku huwa salama dhidi ya maadui na hali mbaya ya hewa.
·         Mfugaji huweza kuwapatia kuku wake virutubisho muhimu na matokeo yake ni ongezeko la uzalishaji.
·         Ni rahisi kudhibiti wadudu na vimelea vinavyosababisha magonjwa kwa kuku.
·         Ni rahisi kuwatenganisha kuku katika makundi tofauti na kuwahudumia ipasavyo.
·         Ni rahisi kutambua kuku wagonjwa na kuwatibu mapema.
·         Kuku hupata mwanga wa jua wa kutosha pamoja na hewa safi na wakati wa jua kali wanaweza kuingia ndani ya banda na kukaa kivulini.
·         Kuku hudhibitiwa wasiharibu mazao na hivyo kuzuia ugomvi na majirani.
·         Upotevu wa kuku na mayai hupungua kwa kiasi kikubwa.
·         Ni rahisi kukusanya na kutumia mbolea ya kuku kwa ajili ya matumizi ya bustani.
·         Ni rahisi kutunza kumbukumbu za ufugaji
·         Ni mfumo mzuri kwa wafugaji wasio na maeneo ya kutosha hasa wafugaji wa mijini

Hasara za mfumo wa nusu huria.
·         Mfugaji atahitaji muda wa ziada kwa ajili ya kuwahudumia kuku kama kuwapa chakula na maji
·         Mfugaji atahitajika kuwatafutia kuku virutubisho vyote muhimu.
·         Linahitajika eneo kubwa kiasi la kufugia.
·         Kuna gharama ya ziada ya kutengeneza banda na wigo na ya kununua au kutengeneza chakula cha kuku.

Mfumo wa ndani ya banda
Kwenye mfumo huu kuku hukaa ndani banda muda wote. Ni mfumo unaotumiwa zaidi na wafugaji wa kuku wa kisasa hasa katika maeneo ya mijini.

Faida za mfumo wa ndani ya banda.
·         Ni rahisi kutambua na kudhibiti magonjwa
·         Ni rahisi kudhibiti upotevu wa kuku, mayai na vifaranga
·         Ni rahisi kuwapatia chakula kulingana na mahitaji yao kwa kila kundi
·         Ni rahisi kuwatambua na kuwaondoa kuku wasiozalisha katika kundi

Changamoto za kufugia ndani ya banda tu
·         Unahitajika muda wa kutosha kuwahudumia kuku
·         Ni mfumo unaoambatana na gharama za kujenga banda na kuwanunulia kuku chakula.
·         Ugonjwa ukiingia ni rahisi kuku kuambukizana.

Ujenzi wa banda bora la kuku
v  Sifa ya banda bora la kuku
·         Liwe imara kuzuia maadui kama panya, vicheche, paka, nyoka na wezi.
·         Liwe na uwezo wa kupitisha hewa na mwanga wa kutosha.
·         Liwe na paa refu na mlango mpana wa kuruhusu mtu mzima kuingia kufanya usafi na kutoa huduma nyingine katika banda kwa uhuru.
·         Kuta na sakafu visiribwe kusiwe na nyufa ili kuondoa maficho ya wadudu kama papasi, viroboto, utitiri n.k.
·         Liwe na ukubwa wa kutosha idadi ya kuku waliopo.
·         Paa liwe imara na lisivuje. Vifaa kama mabati, nyasi, madebe, makuti n.k. vinafaa kutumika kuezeka. Lijengwe mahali pasipotuamisha maji.
·         Lijengwe uelekeo wa Mashariki-Magharibi ili kuzuia mwanga wa jua jua kuingia bandani
Mada: Magonjwa na wadudu wanaoshambulia kuku na jinsi ya kukinga.
  1. Magonjwa ya kuku husababishwa na nini?
Zipo sababu mbalimbali zinazosababisha magonjwa kwa kuku.
·         Magonjwa yanayosababishwa na vimelea vya Bakteria
·         Magonjwa yanayosababishwa na virusi
·         Magonjwa yanayosababishwa na wadudu wa nje ya ngozi
·         Magonjwa yanayosababishwa na minyoo
·         Magonjwa yanayosababishwa na vimelea jamii ya protozoa
·         Magonjwa yanayosababishwa na fangasi na
·         Magonjwa yanayosababishwa na lishe duni

  1. Taja Magonjwa yanayoshambulia kuku?
Magonjwa yanayoshambulia kuku ni mengi na baadhi ni kama yafuatayo

Magonjwa yanayosababishwa na bakteria
  • Taifodi ya kuku (Fowl typhoid)
  • Kuharisha kinyesi cheupe (Bacillary white diarrhea)
  • Kipindupindu cha kuku (Fowl cholera)
  • Mafua ya kuku (Infectious corryza)
  • Kolibasilosis (Colibacillosis)

Magonjwa yanayosababishwa na virusi
  • Mdondo/Kideri/Lufuo (Newcastle Disease)
  • Gumboro (Infectious Bursal Disease)
  • Mareksi (Marek’s Disease)
  • Ndui ya kuku (Fowl pox)

Magonjwa yanayosababishwa na Protozoa
Ugonjwa wa kuhara damu (Coccidiosis)

  1. Taja Wadudu wanaoshambulia kuku?
·         Kupe
·         Papasi
·         Utitiri

  1. Elezea dalili kila ugonjwa?
Dalili za magonjwa ni nyingi na si rahisi kuzielezea kwa kila ugonjwa ila kwa ujumla kuku mgonjwa huonesha dalili zifuatazo:
·         Huonekana mchovu na dhaifu
·         Hula/kunywa kidogo au zaidi ya kawaida
·         Hutoa kamasi puani, ute na matongotongo
·         Huwa na manyoya yaliyo vurugika
·         Hupumua kwa shida au kwa sauti
·         Sehemu ya kutolea haja kubwa huwa na unyevunyevu na wakati mwingine kinyesi hugandia
·         Huharisha na wakati mwingine hutoa kinyesi chenye damu au minyoo
·         Hutaga mayai machache au husimama kutaga kabisa
·         Hujitenga na wenzao katika kundi
·         Husinzia muda wote

  1. Athari za magonjwa?
·         Husababisha kuku kukua taratibu
·         Kuku hupunguza uzalishaji
·         Huwafanya kuku kuwa wadhaifu
·         Husababisha vifo kwa kuku
·         Husabisha hasara kwa mfugaji

  1. Kinga na tiba?
·         Magonjwa ya kuku huweza kukingwa na mengine huweza kutibiwa
·         Kinga
·         Zingatia usafi wa banda na vyombo vya kulia chakula
·         Hakikisha banda linakuwa kavu muda wote
·         Banda liwe na hewa na mwanga wa kutosha
·         Kuku wagonjwa watengwe na kuku wazima
·         Kuwe na dawa ya kunawa miguu ili kuua vijidudu mlangoni (Footbath)
·         Kuku wageni wasichanganywe na kuku waliopo hadi baada ya wiki mbili
·         Kuku wapewe chanjo za kuzuia magonjwa mbalimbali na ratiba ya chanjo izingatiwe

  1. Tiba za asili kama zipo.
Zipo dawa za aina mbalimbali za asili zinazopatikana kwenye mazingira ya vijijini ambazo zinaweza kutibu baadhi ya magonjwa ya kuku. Baadhi ya dawa hizo ni kama zifuatazo:-

Shubiri mwitu (Aloe vera)
Hutumika kutibu magonjwa mbalimbali ya kuku.
Kutibu vidonda vinavyotokana na ndui ya kuku au aina nyingine za vidonda

Maandalizi
  • Chukua majani ya Shubiri mwitu na kuyachana vipande vidogo vidogo.
  • Vitwange na pumba kidogo na kuvianika.
  • Vikikauka vitwange na kuchekecha upate unga laini.
  • Hifadhi unga katika chombo kisafi na kikavu.

Matumizi
Safisha vidonda vilivyotokana na ndui au vidonda vyovyote vile na maji safi yaliyo na chumvi kiasi.
Pakaa unga wa Shubiri mwitu katika vidonda vilivyosafishwa.
Utapakaa unga huu kila siku mpaka vidonda vitakapo pona

Shubiri mwitu pia hutumika kudhibiti magonjwa mengine ya kuku

Maandalizi
  • Chukua jani moja la Shubiri mwitu lenye ukubwa wa wastani.
  • Likate katika vipande vidogo vidogo.
  • Loweka vipande ulivyokata katika maji kiasi cha lita mbili kwa muda wa masaa 12.
Matumizi
Kuku wapewe maji haya wanywe kila siku (Ni muhimu mfugaji kuhakikisha kuwa hakuna maji mengine zaidi ya haya yenye dawa)
Dawa hii inafanya kazi ya kuwakinga kuku dhidi ya magonjwa mbalimbali.
Badilisha maji hayo kabla hayajaanza kuchacha na kuwatengenezea dawa nyingine. Hakikisha chombo kinasafishwa vizuri kabla ya kuwawekea dawa nyingine

Majani ya Mpapai
Hutumika kutibu magonjwa ya kuharisha kwa kuku

Namna ya kuandaa
  • Chukua jani moja bichi la Mpapai na ulipondeponde  lilainike kiasi.
  • Changanya na maji kiasi cha lita mbili na nusu.

Matumizi kwa kutibu
  • Kuku wapewe maji hayo wanywe, wasipewe maji mengine kwa ajili ya kunywa kwa siku angalau nne au zaidi.
  • Inafaa zaidi kila siku kuwaandalia dawa mpya ili dawa isiharibike.

Matumizi kama kinga
Hata kama kuku hawaharishi, wakizoeshwa kunywa maji yenye majani ya mpapai yaliyopondwa angalau mara tatu kwa wiki watakingwa magonjwa mengi.

Mada: Chakula na virutubisho vya kuku
·         Virutubisho vya kuku
Kuku kama ilivyo kwa wanyama wengine wanahitaji virutubisho ili waweze kuwa na afya bora. Vyakula vya kuku ni muhimu kuwa na mchanganyiko wa makundi mbalimbali kama yafuatayo:-
ü  Vyakula vya wanga (Carbohydrates)
ü  Vyakula vya protini (Proteins)
ü  Vyakula vya mafuta (Fats)
ü  Madini na (Minerals)
ü  Vitamini (Vitamins)

·         Material ya kutengeneza chakula cha kuku.
Malighafi zinazohitajika katika kutengeneza vyakula vya kuku ni pamoja na zile zenye mchanganyiko wa makundi ya virutubisho tulivyotaja hapo juu.
ü  Mahindi yaliyoparazwa/Mtama
ü  Pumba za mahindi/Pumba za mpunga
ü  Mashudu ya alizeti/Mashudu ya pamba
ü  Madini mchanganyiko
ü  Chumvi ya mezanio
ü  Chokaa ya mifugo/unga wa mifupa/DCP
ü  Vumbi la dagaa/Dagaa waliosagwa/Damu iliyokaushwa
ü  Vitamini
·         Ratio bora inayotakiwa kutegeneza chakula cha kuku
Yapo makundi mbalimbali ya kuku na kila kundi lina chakula cha aina yake ila kwa ujumla chakula kifutacho kinafaa kwa kuku wanaotaga na kuku wazazi
Aina ya vyakula
Kiasi (Kilo)
Mahindi yaliyo parazwa                                          
8
Mtama
3.5
Pumba ya mahindi                       
3.25
Mashudu ya Alizeti                            
5.5
Dagaa waliosagwa                                                 
4
Chokaa ya mifugo (Au Unga wa mifupa)                                                     
0.75
Madini mchanganyiko                                                  
0.05
Chumvi ya mezani/jikoni                                               
0.05
JUMLA
25

·         Sifa ya chakula bora cha kuku
Chakula bora cha kuku ni kile chenye virutubisho muhimu kwa ajili ya kundi husika la kuku, kwa ujumla kinatakiwa kuwa na mchanganyiko wa Wanga, Protini, Mafuta, Madini na Vitamini. Aidha kuku wapewe maji ya kunywa ambayo ni safi salama muda wote.

Kutaga na kutamia mayai, Elezea
·         Muda wa kuku kuanza kutaga au kuliwa nyama.
Kuku huanza kutaga katika umri tofauti tofauti kulingana na aina ya kuku, kama ni wa kisasa au wa kienyeji. Kwa kawaida kuku wa kisasa huanza kutaga wakiwa na umri wa wiki 18 hadi 22 lakini kuku wa kienyeji wengi wao huanza kutaga wakiwa na umri wa wiki 24. Aidha kuku wa nyama wa kisasa huanza kufaa kwa ajili ya nyama wakiwa na umri wa wiki 7, kuku machotara huweza kufaa kwa ajili ya nyama wakiwa na umri wa miezi mitatu hadi mine. Kuku wa kienyeji kabisa huanza kufaa kuliwa nyama wakiwa na umri wa miezi 5 na kendelea.

·         Jinsi ya kuandaa viota vya kutagia.
Ili kuku aweze kutaga anahitaji sehemu tulivu na iwekwe kiota cha kutagia. Zipo aina nyi8ngi za viota kulingana na uwezo wa mfugaji. Mfugaji anawza kutengeneza viota vya mbao, au kukata boksi, au kukata ndoo na kuvijaza mchanga au kutengeneza viota kwa kutumia nyasi kavu au majani ya mgomba. Ni muhimu kiota kikaandaliwa wakati kuku anapoanza kuonesha dalili za kutaka kuanza kutaga. Kiota kinyunyiziwe dawa ya kudhibiti wadudu au majivu ili kuzuia wadudu wasumbufu kama vile utitiri.

·         Utunzaji bora wa mayai
Mayai yatunzwe sehemu kavu na isiyo na joto kali, boksi liliojazwa mchanga safi au kasha la kuhifadhia mayai linafaa kutumika kwa ajili ya kuhifadhia mayai. Mayai kwa ajili ya kutotolesha yahifadhiwe kwa kuwekwa katika sehemu ya kuhifadhia kwa kuwekwa sehemu butu iwe juu (Sehemu butu ni ile yenye hewa) hii itasaidia kiini tete kuendelea kuwa na uhai. Aidha mayai machafu yasafishwe kwa spiriti ili kusaidia kuua wadudu wa maradhi. Mayai kwa ajili ya kutotolesha yasizidi siku 14 toka kutagwa, yai lililokaa muda mrefu hupoteza uwezo wa kutotolewa

Njia za kutotolesha vifaranga bora, Elezea
Ø  Asilia Kutumia kuku kwa ajili ya kuatamia mayai, kuku waatamiaji wachaguliwe kutoka miongoni mwa kundi na wapewe mayai yasiyozidi 10 kwa ajili ya kuatamia
Ø  TeknolojiaKwa kutumia mashine za kutotolesha mayai (Incubators) 
Ø  Ubunifu  Kwa kutumia pumba za mahindi

Mbinu za kuku kuatamia mayai mengi kwa njia, Elezea
Ø  Asilia Kuku hana uwezo wa kuatamia mayai mengi zaidi ya yale aliyoyataga. Inashauriwa kuku awekewe mayai ambayo ana uwezo wa kuyaatamia na kutotoa vifaranga. Kuku apewe mayai 10 hadi 12 ili aweze kuyaatamia na yote yaweze kufikiwa na joto.

Ø  Teknolojia Zipo teknolojia mbalimbali za kutotolesha mayai, mojawapo ambayo ni maarufu sana ni kwa kutumia mashine za kutotolesha mayai. Zipo mashine za kutumia umeme, mafuta ya taa na sola

Ø  Ubunifu Wafugaji wengi siku hizi wamebuni njia mbalimbali za kutotolesha mayai, baadhi yao hutumia pumba za mahindi kutotolesha mayai. Mayai huwekwa ndani ya pumba na kuachwa kwa muda wa siku 21 kwa ajili ya kutotoleshwa. Njia hizi si za uhakika sana kwani mayai mengi huharibika





Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment